Wawili mbaroni kwa wizi wa miundombinu ya TANESCO Yenye Thamani ya Milioni 61

Wakazi wawili wa Manispaa ya Kinondoni wanashikiliwa na Polisi wakituhumiwa kukutwa na miundombinu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) yenye thamani ya Sh milioni 61.

Walikutwa na miundombinu ya shirika hilo ikiwemo vifaa kwa ajili ya kuunganishia umeme.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lucas Mkondya, alisema watuhumiwa hao walikamatwa juzi saa 10 jioni katika maeneo tofauti ya manispaa hiyo.

Alisema katika tukio la kwanza, maeneo ya Makumbusho, polisi wakishirikiana na kikosi kazi cha kuzuia uharibifu wa miundombinu ya Tanesco, walipata taarifa kutoka kwa raia wema kuhusu kuwepo kwa watu wanaohujumu miundombinu ya shirika hilo.

“Kikosi kazi walifika eneo hilo katika nyumba ya Wilfred Baruti (45) mkazi wa Makumbusho na kufanya upekuzi katika nyumba hiyo na vilipatikana vifaa mbalimbali vinavyotumika kuunganisha umeme vya Tanesco,” alisema Mkondya.

Aidha, alisema pia polisi walikwenda katika nyumba nyingine ya Beatrice Emmanuel (42) mkazi wa Salasala Mabanda Mengi walikofanya upekuzi na kufanikiwa kukamata vifaa ambavyo ni nyaya aina ya drums mbili, rola ya nyaya aina ya AICC ya umeme wa milimeta l ambazo hutumiwa na Tanesco kituo cha Kilimahewa cha Kawe, wilayani Kinondoni.

Alisema upelelezi ukikamilika watafikishwa mahakamani.Mkuu wa kitengo cha mawasiliano Leila Muhaji akizungumza na waandishi wa kuhusu wizi huo wa vifaa vya umeme vyenye thamani ya milioni 61,Kulia ni Kaimu Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam,Lucas Mkondya.

Post a Comment

0 Comments